VITUO MBALIMBALI VYA REDIO VYAENDELEA KUFUNGWA ZANZIBAR KWA KUKIUKA MAADILI
Mkurugenzi wa kituo cha radio cha Swahiba FM, Kassim Suleiman KADHIA ya ufutwaji uchaguzi wa Zanzibar ikiwa haijapatiwa ufumb...
https://samchardtz.blogspot.com/2015/11/vituo-mbalimbali-vya-redio-vyaendelea.html
Mkurugenzi wa kituo cha radio cha Swahiba FM, Kassim Suleiman |
KADHIA
ya ufutwaji uchaguzi wa Zanzibar ikiwa haijapatiwa ufumbuzi, kumekuwa
na hatua za ukandamizaji wa uhuru wa habari hapa Zanzibar na tayari
madhara yametokea. Anaandika Jabir Idrissa, Zanzibar … (endelea).
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilichukua hatua katili tarehe 26 Oktoba
2015, ilipoamuru kufungwa kwa kituo kipya cha redio cha Swahiba FM kwa
maelezo kuwa kimevunja sheria.
Mkurugenzi wa kituo hicho, Kassim Suleiman ameiambia MwanaHALISI Online, kwamba kituo hicho kilifungwa kwa uonevu kwa sababu “hata utaratibu wa kisheria haukufuatwa.”
Kwa mujibu wa Sheria ya Utangazaji ya Zanzibar, amesema hatua kama hiyo
huchukuliwa baada ya mmiliki wa kituo chenyewe kufahamishwa na kuwa
amepewa nafasi rasmi ya kujitetea baada ya kujulishwa kosa linalodaiwa
kuwa limefanywa na kituo.
Kassim ambaye aliwahi kuwa Naibu Mkurugenzi wa Sauti ya Tanzania
Zanzibar (STZ) kabla ya kubadilishwa na kuwa Shirika la Utangazaji la
Zanzibar (ZBC), alisema amelalamika rasmi kwa barua kwa Katibu Mtendaji
wa Tume ya Utangazaji Zanzibar (ZBC).
Kosa lililotajwa kuwa kituo hicho kimefanya ni kutangaza tamko la
Maalim Seif Shariff Hamad la Oktoba 26 la kwamba alikuwa anaonesha kuwa
na kura nyingi na kutaka Tume ya Uchaguzi itangaze matokeo bila ya
kuchelewa.
Taarifa za ndani ya Tume ya Utangazaji zinasema uamuzi huo wa kufunga
kituo cha Swahiba FM, kinachoendeshwa na kampuni inayomilikiwa na Chama
cha Wananchi (CUF), umechukuliwa bila ya Bodi ya Tume kujua.
Kisheria
uamuzi wowote kama huo utachukuliwa baada ya Bodi kujadili tuhuma na
kutoa uamuzi wake. Mjumbe mmoja wa Bodi hiyo ameithibitishia MwanaHALISI
Online, kuwa hawakukaa kujadili suala hilo.
Juzi
askari wa Jeshi la Polisi walivamia maeneo mbalimbali ya mji wa
Zanzibar na kukamata wauza magazeti, na kukamata wafanyakazi wa duka la
vitabu na machapisho la BMC kwa kuwa lilikuwa likitoa nakala za gazeti
la MwanaHALISI la Jumatatu baada ya gazeti hilo kutoonekana mitaani muda
mfupi lipobainika.