Kifungo cha Maisha kwa vigogo wa Khmer Rouge
http://samchardtz.blogspot.com/2014/08/kifungo-cha-maisha-kwa-vigogo-wa-khmer.html
Mahakama ya Cambodia inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa imewahukumu
kifungo cha maisha watu 2 waliokuwa vigogo wa utawala wa Khmer Rouge,
baada ya kuwakuta na hatia ya uhalifu dhidi ya ubinadamu.
Aliyekuwa kiongozi wa Cambodia, Khieu Samphan akisikiliza hukumu dhidi yake
Uamuzi huo wa mahakama umetangazwa leo asubuhi mjini Phnom penh mbele ya
umati wa raia waliofurika mahakamani. Waliokutwa na hatia ndio maafisa
wakuu wa utawala dhalimu wa Khmer Rouge ambao bado wako hai.Wa kwanza ni Nuon Chea mwenye umri wa miaka 88 ambaye pia alifahamika kama Kaka namba mbili kwa kuwa mshirika wa karibu sana na kiongozi wa Khmer Rouge, Pol Pot aliyefariki mwaka 1998. Chea alichukuliwa kama kinara wa mipango ya mauaji ya Khmer Rouge. Wa pili ni Khieu Samphan ambaye alikuwa rais, akiwa kwa wakati huu na umri wa miaka 83.
Nuon Chea a.k.a Kaka namba mbili wakati akisomewa hukumuRufaa dhidi ya kuhumu hiyo
Baada ya hukumu hiyo kutolewa, waliokutwa na hatia hawakutoa kauli yoyote mara moja, lakini baadaye mawakili wao walisema watakata rufaa dhidi ya uamuzi huo, ambao wameuita uonevu dhidi ya wateja wao. Hata hivyo, wakati akitangaza hukumu hiyo, Jaji amesema ingawa rufaa yaweza kukatwa, watu hao watalazimika kubakia gerezani, kutokana na unyeti wa madhambi wanayotuhumiwa kuyafanya.
Baadhi ya wahanga wa ukatili wa utawala wa Khmer rouge waliokuwepo mahakamani wameelezea hisia zao kufuatia hukumu hiyo. ''Tangu mwaka 1979 nimekuwa nikisubiri haki itendeke. Hii ni siku muhimu maishani mwangu.'' Alisema mmoja wao. Mwingine alisema, ''Sitaki kulipiza kisasi, lakini nataka wawataje wauaji wengine walioshirikiana nao.''
Faraja kwa wahanga
Wahanga wa mauaji ya Khmer Rouge wamesema angalau wamefarijikaKaribu robo nzima ya wakazi wote wa Cambodia, takribani watu milioni 1.7 walikuwafa wakati wa utawala wa Khmer Rouge kati ya mwaka 1975-1979. Wengi walikufa kwa njaa, ukosefu wa huduma za afya, kazi ngumu na hata kunyongwa.
Wapo watu wanaoikosoa mahakama hiyo ya Cambodia yenye kuungwa mkono na Umoja wa Mataifa, kutokana na gharama kubwa ya matumizi yake, huku matokeo yakiwa haba.
Ilianza kufanya kazi mwaka 2006, na hadi leo ilikuwa imetumia kiasi cha dola milioni 200 na kukamilisha kesi moja, Kaing Guek Eav aliyekuwa mkuu wa magereza wa utawala wa Khmer Rouge, na ambaye alikutwa na hatia mwaka 2011.
