MAMA WA MTOTO ALBINO ALIYEUAWA AMLIZA JB
Hali si shwari hata kidogo! Wikiendi iliyopita staa wa sinema za Kibongo, Jacob Steven ‘JB’ alijikuta akiangua kilio na kuungwa mkono n...
https://samchardtz.blogspot.com/2015/02/mama-wa-mtoto-albino-aliyeuawa-amliza-jb.html
Hali si shwari hata kidogo! Wikiendi iliyopita staa wa sinema za Kibongo, Jacob Steven ‘JB’ alijikuta akiangua kilio na kuungwa mkono na mastaa wenzake, Amri Athumani ‘Mzee Majuto’ na Single
Mtambalike ‘Richie’ walipomtembelea wodini mama mzazi wa mtoto Albino, Yohana Bahati (1) aliyeuawa kikatili, Ester Thomas (30) ambaye naye alijeruhiwa vibaya kichwani, Ijumaa Wikienda linakuhabarisha.
Walipofika wodini hapo, JB na wenzake walitoa yao ya moyoni kupinga vikali ukatili aliotendewa mama huyo na mwanaye huku wakitahadharisha juu ya laana inayoweza kuikumba jamii yetu kwa tukio hilo.
JB: Nampa pole sana mama Yohana. Hii ni aibu kubwa kwa taifa letu na jamii pana duniani.
Watu hawafanyi kazi kujipatia kipato halali. Mafisadi wanataka kujipatia fedha kupitia njia za kishetani za kuwaua wenzetu. Albino ni wenzetu na tunawapenda. Lazima wahalifu wakamatwe na wahukumiwe kunyongwa.
Mzee Majuto: Inasikitisha sana. Haivumiliki. Albino ni wenzetu na wana uwezo mkubwa wa kulisaidia taifa letu. Wahusila lazima wakamatwe na tuone wakichukuliwa hatua kali.
Richie: Natokwa na machozi. Hiki ni nini? Hatuwezi kufumbia macho jambo hili hasa sisi wenye nafasi kubwa ya kukemea vitendo hivi.
Mara baada ya mastaa hao kutoa la moyoni katika wodi aliyolazwa mama huyo, iligeuka kama msiba kwani kila aliyekuwepo alikuwa akiangua kilio kwa uchungu.
Tayari mtoto Bahati amezikwa baada ya mwili wake kupatikana ukiwa hauna baadhi ya viungo huku mama yake akiendelea na matibabu baada ya kufanyiwa oparesheni sehemu ya kichwani aliyojeruhiwa vibaya wakati akinyang’anywa mwanaye.
KUTOKA KWA MHARIRI
Global Publishers tunaungana na dunia nzima kukemea vikali mauaji ya Albino ambayo rekodi inaonesha hutokea wakati wa uchaguzi mkuu hivyo tunavitaka vyombo husika kufanya kazi yake ili kuliondolea taifa aibu hii nzito.