Flatnews

KENYA: MWENYE GARI LILILOLIPULIWA PANGANI ASHTAKIWA

WASHUKIWA watatu wa ugaidi miongoni mwao mwenye gari lililolipuka katika kituo cha polisi cha Pangani na kusababisha vifo vya watu w...


WASHUKIWA watatu wa ugaidi miongoni mwao mwenye gari lililolipuka katika kituo cha polisi cha Pangani na kusababisha vifo vya watu wanne miongoni mwao maafisa wawili wa polisi walifikishwa mahakamani Ijumaa.


Washukiwa wa Pangani
Washukiwa (kutoka kushoto), Mohamed Abdullahi Falir, Abdiaziz Bulle Ali na Ahmed Dugali Ali wakiwa kortini Nairobi Aprili 25, 2014. Picha/PAUL WAWERU
Hata hivyo hakuna mashtaka yoyote yaliyowasilishwa dhidi ya washukiwa hao ila mahakama iliombwa iwazuilie kwa muda wa siku 10 katika kituo cha polisi cha Muthaiga kusaidia polisi kukamilisha uchunguzi na mahojiano muhimu.
“Washukiwa hawa ni hatari kwa usalama wa kitaifa na maslaha ya umma. Wandani wao bado hawajatiwa nguvuni na wanasakwa na maafisa wa usalama kwa udi na ufumba,”mahakama ilielezwa.
Mabw Ahmed Dugal Ali (mwenye gari lililolipuliwa) , Abdiaziz Bule Ali na Mohammed Abdullahi Falir waliofikishwa mbele ya hakimu mwandamizi Bi Eda Agade chini ya ulinzi mkali katika Mahakama ya Milimani Nairobi hawakutakiwa kujibu mashtaka.

Maafisa wa kitengo cha polisi wa kupambana na ugaidi (ATPU) walisema kwamba wanaume hao wanashukiwa kuwa wanachama wa kundi la kigaidi la Al Shabaab.

Afisa anayechunguza kesi hiyo Bw Cyrus Ikade, alisema katika taarifa aliyoapa na kuwasilisha kortini kuwa washukiwa hao walitiwa nguvuni Aprili 24 kufuatia mlipuko huo ulioshtua wengi.

“Mshukiwa wa kwanza (Ahmed Dugal Ali) ndiye mwenye gari ambapo maafisa hao wawili wa polisi na magaidi wawili walifia,” anasema Bw Ikade na kuongeza, “ Mabw Abdiaziz Bulle Ali na Mohammed Abdullahi Falir wanashukiwa kuwa wandani wa magaidi hao wa Al Shabaab walioangamia katika mlipuko huo.”

Nasaba

Bw Ikade anasema kwamba alimtia nguvuni Bw Ali alipofika katika kituo cha Pangani punde tu mlipuko huo ulipotangazwa na vyombo vya habari na “ kudai ndiye mwenye gari hilo.”

Afisa huyo wa polisi anasema kwamba washukiwa hao wote ni jamaa wamoja na kwamba Abdullahi alishinda siku nzima na magaidi hao kabla ya mlipuko huo kutokea jioni.

Dugal amekana kwamba alikuwa na uhusiano wowote na magaidi hao na kwamba “ yuko tayari kuwasaidia maafisa wa polisi na taarifa yoyote wanayotaka.”

“Naomba hii mahakama ifahamu ninalaani kitendo hivho cha ulipuaji maafisa wa polisi katika kituo cha polisi cha Pangani. Niko tayari kuwasaidi maafisa wa usalama na chochote watakacho,” alisema mahakamani Ijumaa.

Bi Agade alifahamishwa polisi watafanya uchunguzi utakaosambaa hadi Mandera ambapo uraia wao utathibitishwa. Pia polisi watafanya mahojiano zaidi.

Aliomba mahakama iwazuie kwa muda wa siku 10 ndipo uchunguzi ukamilishwe.

Afisa huyo anasema washukiwa hao wanatuhumiwa wanashirikiana na magaidi wanaotekeleza mashambulizi.

Bi Agade alikubalia ombi la maafisa wanaochunguza kesi hiyo na kuamuru washtakiwa wazuiliwe kwa muda wa siku 10.

Hakimu alifahamishwa washtakiwa hao walifikishwa kortini kabla ya masaa 24 kukamilika.

Post a Comment

emo-but-icon

item