SITTI MTEMVU AIPONZA KAMATI YA MISS TANZANIA
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kupitia Baraza la Sanaa la Taifa (Basata), wanatarajia kuifanyia tathmini Kam...
http://samchardtz.blogspot.com/2014/11/sitti-mtemvu-aiponza-kamati-ya-miss.html
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kupitia Baraza la Sanaa la Taifa (Basata), wanatarajia kuifanyia tathmini Kamati ya Miss Tanzania kujua mapungufu yaliyopo ili kuchukua hatua stahiki.
Utata
wa umri wa aliyekuwa mshindi wa taji la mwaka huu, Sitti Mtemvu,
unaonekana kama chanzo cha kuibuka kwa matatizo mengine yaliyokuwa
yakidaiwa kufanyika kinyume cha taratibu za mashindano hayo.
Akizungumza
na Mwananchi jana, Katibu Mkuu Mtendaji wa Basata, Godfrey Mngereza
alisema kwa muda mrefu sasa wamepokea malalamiko tofauti kutoka kwa
wadau yanayoashiria mapungufu makubwa dhidi ya waandaaji hao wa
mashindano ya ulimbwende nchini.
Mngereza
alisema yapo mambo ambayo yanaendelea yanayotakiwa kufanyiwa tathmini
ili kupata picha halisi kabla ya kuyumba na kupoteza sifa kwa mashindano
hayo miaka ijayo.
“Kwa
taratibu zilizopo, Baraza ambalo ndilo lililotoa leseni ya kuendesha
Miss Tanzania litafanya tathmini ili kujua tatizo ni nini na kupata
maoni kutoka kwa wadau kuhusu nini kifanyike au kibadilike ili
mashindano haya yasipoteze sifa, kwani nia yetu kama baraza ni
kuhakikisha tunakuwa miongoni mwa nchi zinazotoa warembo wa dunia na si
kila siku kuangukia pua,”alisema Mngereza.
Akizungumzia
tuhuma zinazowakabili Kamati ya Miss Tanzania, kuhusu kutompa fedha za
maandalizi na michango mingine kwa ajili ya kushiriki Miss World, Miss
Tanzania 2013, Happyness Watimanywa, alisema ni taarifa mpya na
watahakikisha wanazifanyia kazi.
“Hizi
ni taarifa mpya kwa sasa, lakini tutahakikisha tunazifanyia kazi haraka
iwezekanavyo na tutakachoangalia sisi ni mkataba baina yao unasemaje,
tukibaini kwamba waandaaji walikiuka mkataba tutajua kwanini walifanya
hivyo na taratibu zinasemaje hapo ndipo tutajua nini cha kufanya,” alisema.
Mama
mzazi wa Happyness juzi alinukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari
akidai kuwa, mwanaye hakupewa fedha za maandalizi ya mashindano ya Miss
World ilhali alitakiwa kuondoka nchini Jumamosi (jana).
Alifafanua kuwa waandaaji hao wameshindwa kumwandaa katika upande wa mavazi na mengineyo.
Alipotafutwa Hasheem Lundenga, Mkurugenzi wa kampuni ya Lino Agency, alisema: “Suala
hilo halina ukweli wowote, tatizo vyombo vya habari macho yenu ni Miss
Tanzania, na hata hao walioripoti hiyo habari hawajui ukweli kuhusu
taarifa hizo,”alisema Lundenga.
