FCC yakamata shehena ya vipuri bandia vya magari na pikipiki
http://samchardtz.blogspot.com/2014/08/fcc-yakamata-shehena-ya-vipuri-bandia.html
Ofisa Ukaguzi wa Tume ya Ushindani (FCC), Diana Augustino akihesabu
sehemu ya vipuri vya kughushi vya pikipiki vilivyokamatwa katika duka
lililopo Mtaa wa Mahiwa jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki
iliyopita. Aliyeshikilia mfuko ni muhudumu wa duka hilo, Daudi Lucas.
Picha na Nuzulack Dausen
Kazi hiyo ya ukamataji ilifanyika baada ya kuwapo
kwa taarifa za uingizaji wa vipuri vya kuiga kutoka nchini China
vilivyowekwa nembo ya ‘SP Original Piston Ring.’ Vipuri halisi vya nembo
hiyo huingizwa hapa nchini na kampuni ya Saba General Enterprises
pekee.
Dar es Salaam. Tume ya Ushindani (FCC) imekamata
vipuri vya kughushi vya pikipiki vyenye thamani ya zaidi ya Sh23
milioni, katika operesheni ya kushtukiza iliyofanyika katika soko la
Kariakoo jijini hapa.
Kazi hiyo ya ukamataji ilifanyika baada ya kuwapo
kwa taarifa za uingizaji wa vipuri vya kuiga kutoka nchini China
vilivyowekwa nembo ya ‘SP Original Piston Ring.’ Vipuri halisi vya nembo
hiyo huingizwa hapa nchini na kampuni ya Saba General Enterprises
pekee.
Akizungumza baada ya kumaliza operesheni hiyo,
ofisa udhibiti na ukaguzi wa FCC, Emmanuel Ndyetabula alisema walikamata
maboksi 7,912 ya bidhaa hizo katika duka na ghala linalomilikiwa na
Anania Tweve. Kila boksi moja la vipuri hivyo huuzwa kwa bei ya jumla ya
Sh3,000.
Maofisa wa FCC na polisi wa Kituo cha Msimbazi
walikamata pia sehemu ya vipuri hivyo ndani ya duka lijulikanalo kwa
jina la Jezetwe Motorcyle and Spare Parts lililopo Mtaa wa Nyamwezi na
Mafia.
Sehemu nyingine kubwa ya vipuri ilikamatwa katika ghala la duka hilo lililopo Mtaa wa Mahiwa.
Ndyetabula alisema licha ya kuwapo na ongezeko la
kubwa la uuzaji wa vipuri vya kughushi vya magari na pikipiki nchini,
hii ni mara ya kwanza kwao kukamata vipuri vingi kiasi hicho kwa wakati
mmoja.
“Hawa jamaa ni wajanja sana.dukani kwao wameweka
bidhaa za nembo nyingine zinazofanana na SP na iwapo mteja akiulizia
nembo hiyo basi hupanda juu ya dali kwenda kumchukulia. Baada ya
uchunguzi na maofisa wa Saba General, tulibaini wana ghala kubwa ambalo
huzihifadhi na kuziuza kwa kificho,” alisema Ndyetabula. Ofisa wa Saba
General alisema mauzo ya vipuri hivyo yamekuwa yakishuka licha ya
mahitaji kuongezeka.
“Baada ya kushuka kwa mauzo ilibidi timu yetu
ianze kuchunguza chanzo ni nini, ndipo tukabaini kuna wafanyabiashara
wanaingiza bidhaa feki kutoka China na kuziuza kwa bei ndogo,” alisema.
Alisema ili kuzitofautisha na bidhaa halisi za Sp
piston ring, feki hazijaandikwa namba ya uzalishaji kwenye boksi na
ndani vina rangi nyeusi badala ya rangi ya fedha. “Hivi vipuri bandia
ukitumia siku tatu tu vinaanza kuvujisha moshi,” alisema.
Ofisa huyo alisema wao huuza vipuri hivyo kwa bei
ya jumla ya Sh3,500 kwa boksi lakini wauzaji wanaouza bandia huuza kwa
maelewano huku bei mara nyingi ikiwa kati ya Sh2,000 na Sh3,000.
Muuzaji wa duka hilo, Fadhili Tweve alisema hafahamu vipuri hivyo vilikonunuliwa bali bosi wake ndiye anayejua mchakato mzima.
Ndyetabula aliwataka Watanzania na Kampuni
zinazozalisha au kufanya uwakala wa bidhaa mbalimbali nchini
kushirikiana na FCC ili kutokomeza bidhaa bandia.