Flatnews

Hata mnyama anaona soni

Mackie Mdachi  Kwa ufupi Mwanadamu ambaye anakosa kabisa ‘hali’ hiyo hapo juu, je, tunamfana...


Mackie Mdachi 
Kwa ufupi
Mwanadamu ambaye anakosa kabisa ‘hali’ hiyo hapo juu, je, tunamfananisha na kitu gani.  Au tumweke kwenye fungu gani?  Na mara nyingi watu wa aina hiyo tabia zao ni aidha za ucheshi, upole na kuonyesha aina ya kujipendekeza kwa wanajamii yaani ni wanafiki au wazandiki-haswa.


Soni inaelelzwa ni ‘aibu, haya’, yaani tabia au hali ya mtu kuogopa maovu au aibu yake isijulikane na watu.  Fedheha, hali ya kusitasita kusema au kufanya jambo kwa sababu ya kumheshimu mtu mwingine.  Hali ya kutoweza kumwangalia au kuangalia mtu machoni.
Mwanadamu ambaye anakosa kabisa ‘hali’ hiyo hapo juu, je, tunamfananisha na kitu gani.  Au tumweke kwenye fungu gani?  Na mara nyingi watu wa aina hiyo tabia zao ni aidha za ucheshi, upole na kuonyesha aina ya kujipendekeza kwa wanajamii yaani ni wanafiki au wazandiki-haswa.
Ukutanapo ghafla na simba porini, wawindaji hata wana vijiji wanathibitisha ya kuwa mnyama huyo huinamisha kichwa chake chini au hugeuka upande mwingine kwa soni na kutokomea porini.  Vivyo hivyo hata paka umkutapo jikoni amefunua chungu na kula kitoweo, naye ghafla hukuangalia kwa soni na kuondoka jikoni.
Yawaje wewe kiongozi wa umma ukakosa soni kabisa?  Sisiti kabisa kusema wahusika wote wa kashfa ya wizi wa kujitakia wenyewe ya IPTL-Escrow wasionewe ‘haya’ wala kusamehewa kwani hiyo siyo ajali; na wala zile lugha za ‘ajali ya kisiasa zisiwepo asilaani; ukiwa ‘umehomola’ kisicho stahiki yako, wewe ni mwizi tu.
Ya-Musa na Firauni
Hadithi ya Musa ni njema yenye upendo huruma, kuwajali na kuwathamini wanajamii wenzake Wana-Israeli, wakiwa katika dhiki, umaskini, utumwa na mateso nchini Misri; chini ya himaya ya Farao almaarufu Firauni.  Naye Firauni pasina ‘soni’ ya aina yoyote ile aliwatesa Wana Israeli. Soma Biblia-Kitabu cha Kutoka 3-10.
Hadithi hii inafanana na juhudi zilizofanywa na waasisi wa taifa letu, hayati Mwalimu Julius K. Nyerere-Musa na baadhi ya wenzake; ghafla tunakutana na ma-Firauni ni aibu mno na inasononyesha jamii yote ya Watanzania ambao kila uchwapo wanapigana na maisha duni waliyonayo pamoja na utajiri mkubwa walionao wa maliasili kadhaa nchini; ambazo zinaliwa na wachache mchana kweupee.
Si-hao tu waliochota mabilioni ya fedha ilhali wakijua ni fedha za umma, kwani hazikudondoka kutoka mtini au mbinguni kwa ajili yao; wapo pia wapiga debe wao wa waziwazi waliwatetea kwa nguvu zote; nao kwa kivuli ati cha kukinusuru chama na Serikali.  Ebo! Nao pia hawana ‘soni’ wanapindisha sheria na ndimi zao.
Chama kinaweza kuwapo hiki na kile na kingine tena, lakini wanajamii yaani Wananchi ni wale wale ambao wanaendelea kuzongwa na uhaba wa dawa, madawati, vyumba vya madarasa, maabara, kipato duni, kukosa soko thabiti la mazao yao, elimu isiyokidhi, walimu kukosa mishahara kwa wakati, kutopandishwa vyeo wafanyakazi, uhaba wa maji, umeme wa mashaka na vinginevyo hata maji yasiyo salama.
Kwa hali hiyo bado wapiga debe na hao wezi wa fedha za umma Tegeta-Escrow wanajifanya hamnazo na kuona ni haki yao kutoka kwa ‘mungu’ wao dhidi ya wanajamii wote wa Tanzania.

Related

H/KITAIFA 149940649962094776

Post a Comment

emo-but-icon

item