Gharama za maisha zapaa Samunge
https://samchardtz.blogspot.com/2014/05/gharama-za-maisha-zapaa-samunge.html
Maelfu ya
vijana kutoka sehemu mbalimbali nchini wapo Samunge kuchimba dhahabu
katika Mto uliokauka wa Karabaline huku wakisema wanapata dhahabu yenye
ubora wa juu kuliko ya mahali pengine.
Gharama
za maisha katika Kijiji cha Samunge wilayani Loliondo ambako maelfu ya
watu wamekimbilia kuchimba dhahabu ambayo imegundulika, zimepanda
kiwango cha kutisha hasa chakula na maji.
Katika
machimbo hayo mapya maji yanapatikana mbali na eneo hilo, hivyo kufanya
ndoo moja ya maji kuuzwa kati ya Sh500 na Sh2,000.
Maji
katika eneo hilo lililotapakaa machimbo madogo yasiyo rasmi,
yanasambazwa kwa kutumia punda ambao husafiri umbali mrefu na maji hayo
pia hutumika kusafishia dhahabu kwa kuwa mto ambao madini hayo
yanapatikana umeshakauka.
Kwa
upande wa chakula, sahani ya wali inauzwa kati ya Sh3,000 na Sh6,000
huku mguu wa mbuzi ambao wanachinjwa hapo kwa wingi ni Sh8,000.
Mchungaji Mwasapila anena
Akizungumzia
hali hiyo jana, Mchungaji Ambilikile Mwasapila aliiomba Serikali kuweka
utaratibu wa wachimbaji hao kupata maji ili kazi yao isisimame.
Mwasapila
aliyewahi kukaririwa akisema watu watajaa tena Samunge kuliko wale
waliokwenda kwake kunywa kikombe cha dawa ya kutibu magonjwa sugu,
alisema kupatikana kwa dhahabu katika eneo hilo ni sehemu tu ya ndoto
yake.
Alisema
mbali na dhahabu hiyo ya Samunge inayoanza kukusanya watu, bado kuna
mambo makubwa yatakayotokea na maelfu ya watu kujaa zaidi.
"Hili la dhahabu sijawahi kulisema lakini kuna mengi yatatokea katika eneo hili la Samunge," alisema.
Kama
ilivyokuwa wakati wa tiba hiyo, katika machimbo haya bado hakuna mahala
pa kulala, wachimbaji na watoa huduma katika eneo hilo wanalala kwenye
mahema na kijijini Samunge.
Huduma za afya zinapatikana jirani na eneo la machimbo ambako safari hii kuna zahanati.