BUNGE LAPITISHA BAJETI YA WIZARA YA UJENZI 2014/2015
https://samchardtz.blogspot.com/2014/05/bunge-lapitisha-bajeti-ya-wizara-ya.html
Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo limepitisha Bajeti ya Wizara ya
Ujenzi yenye jumla ya Shilingi 1,219,717,592,000.00 kwa ajili ya
matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2014/15.
Hatua
hiyo ya Bunge kupitisha Bajeti hiyo itawezesha Wizara ya Ujenzi
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kuendeleza Sekta ya Ujenzi hapa
nchini.
Akiwasilisha
hotuba ya bajeti hiyo jana, Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe
Magufuli (Mb), alieleza kuwa kati ya fedha hizo Shilingi
557,483,563,000.00 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida ambazo
zinajumuisha Shilingi 24,338,319,000.00 za mishahara ya Watumishi (PE),
Shilingi 6,944,846,000.00 za matumizi mengineyo (OC) na Shilingi
526,200,400,000.00 kwa ajili ya Mfuko wa Barabara.
Akifafanua
kuhusu bajeti ya Maendeleo iliyotengewa Shilingi 662,234,027,000.00,
Mhe. Magufuli ameeleza kuwa, kati ya fedha hizo Shilingi
450,000,000,000.00 ni fedha za ndani za miradi ya maendeleo na Shilingi
212,234,027,000.00 ni fedha za nje za miradi ya maendeleo.
Wizara ya
Ujenzi ina majukumu yafuatayo, Kusimamia Sera za ujenzi na usalama
barabarani, Ujenzi na matengenezo ya barabara, madaraja na vivuko.
Pamoja na
majukumu hayo Wizara pia inasimamia ukarabati wa majengo ya Serikali,
huduma za Ufundi na umeme, kusimamia shughuli za usajili wa Makandarasi,
Wahandisi, Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi, Usalama barabarani
na mazingira katika sekta hiyo.
Pia
Wizara inasimamia uboreshaji, utendaji na uendelezaji wa watumishi wa
Wizara pamoja na kusimamia utekelezaji wa majukumu ya Wakala,Taasisi na
Bodi zilizo chini ya Wizara.