Magufuli ahimiza Daraja Kigamboni
http://samchardtz.blogspot.com/2014/08/magufuli-ahimiza-daraja-kigamboni.html
NAKAGUA: Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli akipata maelekezo kutoka kwa
Meneja Mradi wa Daraja la Kigamboni, Mhandisi Karim Mattaka (kushoto)
wakati wa ziara ya waziri huyo kukagua ujenzi wa daraja hilo na vivuko
jijini Dar es Salaam jana. Picha na Venance Nestory
- Dk Magufuli amewamwagia sifa wakandarasi wazawa akisema wanaweza kufanya kazi vizuri kuliko wakandarasi wa kigeni wanapoaminiwa na kupewa miradi ili waitekeleze.
Dar es Salaam.
Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli amewataka watendaji na wakandarasi
wanaojenga Daraja la Kigamboni, kuhakikisha wanakamilisha ujenzi huo
kabla ya Juni mwakani.
Pia, Dk Magufuli amewamwagia sifa wakandarasi
wazawa akisema wanaweza kufanya kazi vizuri kuliko wakandarasi wa kigeni
wanapoaminiwa na kupewa miradi ili waitekeleze.
Magufuli aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam
wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua Kivuko cha Msanga Mkuu, mkoani
Mtwara kinachojengwa, Kivuko cha Kigamboni kinachofanyiwa ukarabati na
Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kamandi ya Wanamaji na ukaguzi wa
Daraja la Kigamboni.
Daraja hilo linalojengwa na kampuni ya Kichina
ujenzi wake unaelezwa kuwa umekamilika kwa asilimia 60, huku barabara
zake zikiwa zimejengwa kwa asilimia 37, ambapo takriban Sh214 bilioni
zitatumika kukamilisha ujenzi huo ulioanza mwaka 2012 ukitarajiwa
kukamilika Januari mwakani kwa fedha za Serikali na Shirika la Hifadhi
za Jamii (NSSF).
“Ninawaomba watendaji na makandarasi wote na NSSF
mfanye kazi usiku na mchana ili kuhakikisha inapofika Juni mwakani na
siyo Julai mlivyosema, daraja hili liwe limekamilika na Rais Jakaya
Kikwete aje hapa alifungue yeye mwenyewe kwani ndiye aliyelianzisha,”
alisema Dk Magufuli
Kuhusu makandarasi wa ndani, Dk Magufuli alisema
Kampuni ya Uholanzi ya Schepsbouw Noord, ilipewa kujenga kivuko cha
Msanga Mkuu, lakini kwa kipindi cha miaka mitatu ilishindwa
kukikamilisha hivyo alifukuzwa na kazi hiyo kukabidhiwa mkandarasi
mzalendo. “Wazalendo wanaweza, hawa Wazungu hawafai kabisa…,” alisikika
akisema Dk Magufuli.
Awali Meneja Mradi wa Daraja la Kigamboni, Mhandisi Karim Mattaka alisema mpaka sasa jumla ya Sh117 zimetumika.