KOCHA TAIFA STARS ASHAURI KUPUNGUZA IDADI YA WACHEZAJI WA KIGENI LIGI KUU BARA
http://samchardtz.blogspot.com/2014/08/kocha-taifa-stars-ashauri-kupunguza.html
Kocha wa zamani wa Taifa Stars, Dr. Mshindo Msolla
KOCHA mkuu wa zamani wa timu ya taifa ya Tanzania,
Mzalendo, Mshindo Msolla amesema walimu wa kigeni wanaokuja nchini kufundisha
klabu kubwa za ligi kuu hawasaidii kuendeleza soka la Tanzania.
Msolla alisema makocha hawa wanapewa mkataba wa
mwaka mmoja au miwili, hivyo wanahangaika kusajili wachezaji nyota wa kigeni
ili kupata mafanikio na kuondoka, jambo ambalo linawanyima nafasi ya kuwajenga
wachezaji wazawa kwa muda mrefu.
“Hawa walimu wa kigeni wanaokuja klabu zetu kubwa,
hawatusaidii kuendeleza mpirawetu.
Katika mkataba wake wa miaka miwili anataka afanikiwe aondoke. Kwa mfano yule kocha
wa Yanga, Costadin Papic alitaka kila nyota aletwe”
“Labda naona kidogo Maximo anajitahidi. TFF wao
ndio wasimamizi wa mpira, wasichanganyikiwe kwa timu ya taifa kutolewa katika
mashindano ya kufuzu fainali za Afrika, wakubali kwasababu hatuna mipango
endelevu”.
Kocha huyo aliyeifundisha Taifa Stars mara nyingi
kwa vipindi tofauti na mara ya mwisho ilikuwa mwaka 2005 kabla ya kuja kwa Marcio Maximo 2006 aliongeza kuwa idadi kubwa ya wachezaji
wa kigeni (watano) inasababisha kuathiri timu ya taifa kwasababu wanakuja kuwabana
wazawa kupata nafasi ya kucheza.

“Timu ya taifa ya Tanzania imeathirika kwasababu
ya haya, tumeng`ang`ania kuwa na wachezaji wengi wa kigeni, nikiangalia usajili
wa mwaka huu ulivyo kwa timu kubwa tatu (Yanga, Simba na Azam fc), inawezekana
kwenye safu ya ushambuliaji wa timu hizi, mchezaji mmoja wa Kitanzania akawepo,
haitasaidia kuwajenga Watanzania.” Alisema Msolla.
“Kama una timu tatu zinazotoa wachezaji wa timu ya
taifa, halafu katika timu hizo ni mchezaji mmoja tu anayeanza, haiwezi kusaidia.
Ushauri wangu idadi ya wachezaji wa kigeni isizidi watatu.”
Msolla alitoa ushauri kwa shirikisho la soka
Tanzania, TFF, kuwatumia makocha wazawa waliowahi kufundisha timu ya taifa ili
wawe wanampa ushauri kwa kwasababu ya uzoefu wao wa soka la Tanzania.
“Pale TFF kuna kamati ya ufundi na mkurugenzi wa
ufundi. Mimi nilishauri, nchi hii ina walimu wengi wazawa waliofundisha timu ya
taifa , mwalimu wa timu ya taifa hatapoteza chochote kama tutakaa naye kuweka
mipango. Yaani sisi tumsaidie kwasababu
tunawajua wachezaji wetu, na hili halina gharama yoyote.” Alisema Msolla.
“Mwalimu sio mungu, hatutamlazimisha amchague
nani, lakini tunamshauri tu na hii itasaidia kwasababu sisi tunawajua wachezaji
wetu”.
